Mbunge wa Kigamboni Alalamika KERO za Wananchi Kupuuzwa Daraja la Nyerere

Mbunge wa Kigamboni Faustine Ndugulile (CCM) amekua akipokea kero mbalimbali za wakazi wa Kigamboni ikiwemo kiwango kikubwa cha pesa kinachotozwa pale tu wanapopita na magari kwenye daraja hilo, kazifanyia kazi kwa kuzifikisha kunakotakiwa na maelezo yake ndio haya hapa chini.

"Kwa muda mrefu nimekuwa nikipokea malalamiko ya wananchi kuhusiana na huduma isiyoridhisha kwenye Daraja la Nyerere linalounganisha Kigamboni na Kurasini.

Malalamiko ya wananchi yako kwenye maeneo makuu matatu:

1. Kutumika kwa madirisha machache ya kukatia tiketi. Daraja la Nyerere lina madirisha 14 ( Saba wakati wa kuingia na Saba wakati wa kutokea). Madirisha yanayotumika ni machache na hivyo kusababisha foleni isiyo na msingi.

2. Tozo za Daraja la Nyerere zipo juu sana hususan kwa magari ya abiria hali hii imepelekea Kigamboni kukosa ruti ndefu za kuelekea maeneo mengine ya Jiji la Dar Es Salaam, gari la abiria linatozwa kati ya Tsh 5000-7000 kwa kila safari ambayo ni gharama kubwa sana kwa kutwa.

3. Kutokamilika kwa kipande kilichobaki toka Darajani hadi kwa Msomali.

Kama Mbunge wa Kigamboni nimekuwa nikifuatilia suala hili kwa karibu sana bila ya mafanikio, tukumbuke kuwa Daraja la Nyerere lilizinduliwa tarehe 19.04.2016 na sasa ni zaidi ya miezi 9 hamna kinachoendelea na wahusika hawatoi majibu yanayotosheleza.

HATUA NILIZOCHUKUA HADI HIVI SASA

1. Mnamo tarehe 15.06.2016 nilimwandikia barua Waziri wa Ujenzi Mhe. Makame Mbarawa (Mb) kuhusiana na hoja hizi pamoja na kufatilia zaidi ya mara kumi kwa simu, maongezi ya ana kwa ana na meseji, barua yangu haijajibiwa hadi hivi sasa (Angalia kiambatanisho).

2. Vilevile nilikutana na Mkurugenzi wa NSSF Prog Godius Kahyarara tarehe 3.10.2016 kuhusu hoja tajwa hapo juu, aliahidi kuchukua hatua za haraka lakini hadi hivi sasa hakuna kilichofanyika.

3. Kwa kuwa usimamizi wa Daraja la Nyerere upo chini ya NSSF na kipande kilichobaki kitajengwa na NSSF, niliomba kukutana na Waziri anayesimamia taasisi hii, nilikutana na Waziri Jenista Mhagama (Mb) tarehe 3.12.2016 ofisini kwake.

"Pamoja na maelezo ya mdomo, nilimkabidhi barua ya malalamiko (Angalia kiambatanisho), Waziri aliahidi kuchukua hatua za haraka.

"Tarehe 13.12.2016 nilipata nakala ya barua aliyoandika Mhe. Waziri Mhagama kwenda kwa Mkurugenzi Mkuu wa NSSF ili kupata maelezo na ufumbuzi wa hoja nilizotoa, pamoja na kukumbushia Mhe. Waziri Mhagama hajanipatia majibu ya hoja zangu.

"Aidha, maelezo niliyopata toka kwa Mkurugenzi wa NSSF wakati Waziri Mkuu anatembelea Kigamboni tarehe 04.01.2017 ni kwamba fedha zinazohitajika kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa kipande kilichobaki ni Tsh 24 Bilioni na alinihakikishia kuwa FEDHA HIZO ZIPO.

"Michoro (design) ya barabara hiyo IMESHAKAMILIKA, Mkandarasi kwa ajili ya kazi hiyo YUPO

"Pamoja na NSSF kuwa na fedha ya ujenzi wa barabara hiyo, mkandarasi aliye tayari na michoro iliyokamilika, kumekuwa na kigugumizi ya lini kazi hii itaanza inasikitisha pia kuona Mawaziri hawajibu barua pamoja na kukumbushwa mara kwa mara.

"Kinachoendelea sasa hakuna lugha nyingine ya kuielezea zaidi ya UZEMBE na KUTOWAJIBIKA, naleta taarifa hii kwenu wakazi wa Kigamboni ili nanyi mjue kinachoendelea, ninakusudia kuyapeleka malalamiko yenu kwa mamlaka ya juu zaidi baada ya mamlaka tajwa hapo juu kushindwa kupata ufumbuzi."

No comments

Content by MwasebaINFO.All RIghts Reserved. Powered by Blogger.