Polisi Pwani wakamata SMG na risasi 14

KAMANDA WA POLISI MKOA WA PWANI, BONAVENTURA MUSHONGI.

POLISI mkoa wa Pwani inamshikilia fundi ujenzi Khalid Mohamed (29), mkazi wa Kibaha kwa Mathias akiwa na silaha aina ya SMG na risasi 14.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Bonaventura Mushongi, aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa mtuhumiwa huyo walimkamata juzi jioni huko Misugusugu na alikutwa na risasi nne za bunduki aina ya shotgun, mlipuko mmoja, sime na kinyago cha kufunika usoni.

Alisema vitu hivyo walivyomkamata navyo vilihifadhiwa kwenye mfuko wa rambo ukiwa umefukiwa ardhini kwenye shamba la mmiliki aliyetajwa kwa jina la moja la Swai.

Kamanda Mushongi alisema uchunguzi wa awali umebaini kuwa, mtuhumiwa huyo na wengine 15 wanaoshikiliwa la jeshi hilo wanahusika na matukio ya uporaji katika maeneo mbalimbali mkoani hapa likiwemo la mauaji la aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Liwale mwaka 2012, Ephraim Mbaga.

Alisema mkuu huyo wa zamani wa wilaya aliuawa akiwa nyumbani kwake kwa kupigwa risasi mguu wa kushoto na pia kujeruhiwa kwa kitu chenye ncha kali na kufariki wakati akipelekwa Hospitali ya Rufani ya Tumbi mkoani humo. Mushongi alisema watuhumiwa hao wamekiri kuhusika na matukio hayo.

No comments

Content by MwasebaINFO.All RIghts Reserved. Powered by Blogger.