Majaliwa aagiza uchunguzi kubaini shida ya elimu Mtwara

WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa ameziagiza Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya na Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) kwenda mkoani Mtwara na kufanya uchunguzi wa kina ii kubaini sababu za mkoa huo kushika mkia katika matokeo ya upimaji wa wanafunzi wa kidato cha pili.

Majaliwa aliyekuwa mkoani Katavi kwa ziara maalumu alitoa agizo hilo muda mfupi kabla hajafungua rasmi duka la dawa lililojengwa katika Hospitali ya Manispaa ya Mpanda huku akiuliza “kwa nini Mtwara?”

Alisema lazima zipo sababu za mkoa huo kufanya vibaya katika matokeo ya mtihani huo hivyo kuna ulazima wa wizara hizo mbili kwenda mkoani humo kufanya uchunguzi wa kina ili kuzibaini sababu hizo.

“Haiwezekani kwa shule kumi nchini zilizoshika mkia kati ya hizo shule tisa zikitoka katika mkoa mmoja lazima kuna sababu ...naziagiza Wizara ya Elimu na Ufundi Stadi na Tamisemi kwenda mkoani Mtwara na kufanya uchunguzi wa kina ili ziweze kujua kuna nini ….kwa nini Mtwara,” alihoji Waziri Mkuu.

Aliupongeza Mkoa wa Katavi kwa kushika nafasi ya pili kitaifa baada ya Mkoa wa Geita kwa kufanya vizuri katika matokeo ya Taifa wa kumaliza Elimu ya Msingi mwaka 2016 huku akiziagiza halmashauri nchini kupitia idara ya ukaguzi kuhakikisha shule na walimu wanakaguliwa mara kwa mara ili kuongeza ubora utoaji wa elimu.

Awali, akisoma taarifa ya mkoa, Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Raphael Muhuga alimweleza Waziri Mkuu kuwa kwa miaka kadhaa mkoa huo umekuwa ukishika nafasi ya kwanza nchini katika matokeo ya mtihani wa kitaifa wa kuhitimu Elimu ya Msingi nchini, na kwamba wamejipanga kuhakikisha mwaka huu wanarejea kileleni.

No comments

Content by MwasebaINFO.All RIghts Reserved. Powered by Blogger.